Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kiteto, CPA. Hawa Abdul Hassan, amewapongeza kwa dhati walimu na watendaji wote wa sekta ya elimu wilayani hapa kwa jitihada, kujitoa na moyo wa uzalendo uliosaidia kuleta mabadiliko makubwa ya ufaulu katika Mtihani wa Taifa wa Kidato cha Nne 2025.
Akizungumza kufuatia kutangazwa kwa matokeo ya mtihani huo uliofanyika Novemba 2025, CPA. Hawa amesema mafanikio hayo si ya bahati nasibu, bali ni matokeo ya kazi kubwa inayofanywa na walimu kwa kushirikiana na serikali pamoja na wadau wa elimu, kwa lengo la kuhakikisha watoto wa Kiteto wanapata elimu bora na yenye ushindani.
“Nawapongeza sana Walimu wangu mahiri kwa jitihada kubwa kutufikisha hapa. Ninathamini sana jitihada zao na kujitoa kwao,” amesema CPA. Hawa.
Katika matokeo hayo, Halmashauri ya Wilaya ya Kiteto imeongeza ufaulu kutoka asilimia 92.9 mwaka 2024 hadi asilimia 97.8 mwaka 2025, hatua inayothibitisha kupanda kwa kiwango cha taaluma na ufanisi wa mikakati iliyowekwa katika sekta ya elimu.
Akielezea sababu za mafanikio hayo, Mkuu wa Divisheni ya Sekondari wilayani Kiteto, Mwl. Ally Kichuri, amesema ongezeko hilo limetokana na juhudi za makusudi za Serikali katika kuboresha miundombinu ya elimu pamoja na kuimarisha rasilimali watu.
“Mbali na kuboresha miundombinu ya elimu, mafanikio haya yamepatikana baada ya serikali kuajiri walimu wapya, jambo lililopunguza kwa kiasi kikubwa uhaba wa walimu wilayani hapa,” amesema Mwl. Kichuri.
Kwa kuangalia mwenendo wa ufaulu kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo, Kiteto imeonesha safari ya maendeleo yenye mwelekeo chanya na wa kudumu. Mwaka 2023 ufaulu ulikuwa asilimia 90.6, mwaka 2024 ukaongezeka hadi asilimia 92.9, huku mwaka 2025 ukifikia asilimia 97.8. Ongezeko hili linaonesha kuwa uwekezaji katika elimu, usimamizi thabiti na moyo wa kujitoa kwa walimu vinaendelea kuzaa matunda yanayoonekana wazi.
Kwa mafanikio haya, Kiteto haijaongeza tu asilimia za ufaulu, bali imeimarisha imani ya jamii kuwa elimu ni nyenzo muhimu ya mabadiliko ya kijamii na kiuchumi, huku walimu wakibaki kuwa nguzo kuu ya safari hiyo ya mafanikio.
Katika matokeo hayo, Mkoa wa Manyara u eshika nafasi ya pili kati ya mikoa 31 kitaifa, jambo ambalo linaupa mkoa heshima na hadhi katika sekta ya elimu nchini.
Kibaya-Kiteto
Anwani ya Posta: P.o.Box 98, Kibaya-Kiteto
Simu ya Mezani: +255 027-2552099
Simu ya kiganjani:
Barua Pepe: ded@kitetodc.go.tz
Hakimiliki@2017 Halimashauri ya Kiteto.Haki zote zimehifadhiwa