Mbunge wa Kiteto Mhe. Emmanuel Papian akizungumza na wakazi wa kijiji cha Mbigiri katika mkutano wa hadhara uliofanyika kijijini hapo mwishoni mwa wiki.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Mbigiri akifungua Mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji cha Mbigiri mwishoni mwa wiki.
Wakazi wa kijiji cha Mbigiri wakiwa wamekusanyika kumsikiliza Mbunge wao Mhe. Emanuel Papian katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji cha Mbigiri mwishoni mwa wiki.
Wakazi wa kijiji cha Mbigiri wakiwasilisha kero kwa Mbunge wao Mhe. Emanuel Papian katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji cha Mbigiri mwishoni mwa wiki.
........... HABARI KAMILI.........
Mbunge wa Kiteto Mheshimwa Emmanuel Papian amewahimiza wakazi wa kijiji cha Mbigiri kushiriki katika kupanga namna ya kujenga na kuchangia ujenzi wa Zahanati ya kijiji chao , ili waondokane na usumbufu wa kwenda kufuata huduma za afya mbali .Mhe. Papian ameyasema hayo wakati akizungumza na wanajiji hao katika mkutano wa hadhara uliofanyika kijijini hapo mwishoni mwa wiki.
Akizungumza katika mkutano huo Mhe. Papian amewataka wanakijiji hao kujitokeza kushiriki katika mkutano mkuu wa kijiji utakaoitishwa ili kuweza kujadili namna ya kuchangia ujenzi wa Zahanati ya kijiji hicho , na yeye mwenyewe akiahidi kushiriki katika kuchangia ujenzi huo. Mhe. Papian amesisitiza kuhusu wanakijiji hao kuchangia ujenzi wa zahanati hiyo, na hapa anasema “Wananchi wote mjitokeze na mshiriki, kuhakikisha kwamba mnapanga bajeti itakayotosheleza kujenga zahanati hiyo. Na kwa sababu ni msimu wa mavuno sasa, ni vema utekelezaji wa jambo hili ukawa wa haraka, na mimi nitashiriki kuchangia ili tupate zahanati , muweze kutibiwa hapa”.
Kadhalika Mhe. Papian ametoa angalizo kwa wakazi wa kijiji wa hicho kujiwekea akiba ya chakula msimu huu wa mavuno, ili chakula hicho kiweze kuwasaidia kwa wakati wote,hadi watakapovuna tena,kwani serikali imeshatoa agizo kwamba watu wahifadhi chakula kwa sababu hakutakuwa na chakula cha msaada.
Akisisitiza kuhusu wanakijiji hao kuhifadhi chakula Mhe. Papian amesema“ Kila mtu ahakikishe anahifadhi chakula chakutosha nyumbani kwake,kama hukulima,kalime miraba, nunua chakula weka ndani.Kama umelima uza kiasi,mengine hifadhi kwa ajili ya chakula mpaka mwakani,hakuna chakula cha msaada Tanzania. Msije mkatumia mavuno yote,halafu mkategemea chakula cha msaada,hakipo,hifadhini chakula cha kutosha”.
Katika mkutano huo, wanakijiji wamewasilisha kero mbalimbali kwa Mhe. Mbunge ,miongoni mwa kero hizo ni wananchi kuchangishwa fedha kiasi cha sh. 20,000 kwa ajili ya kupimiwa na kupewa viwanja, ambapo hadi wakati huu hawajapewa viwanja hivyo. Ukosefu wa huduma ya maji, ambapo maji yako umbali mrefu sana kutoka kijijini hapo kiasi ambacho wananchi hawawezi kubeba ndoo kwa kichwa, hali ambayo inayowasababisha kununua maji yanayoletwa na magari ( Maboza) huku ndoo moja ya lita ishirini ikiuzwa kati ya. shilingi 400 – 500, na uchungiaji mifugo katika mashamba,ambapo kero hiyo inasababisha usumbufu mkubwa kwa wakulima .
Mhe. Papian ametoa majibu ya kero hizo ambapo katika kero ya viwanja amewataka wananchi wote wenye risiti za malipo kwa ajili ya kupimiwa viwanja waende na risiti zao katika ofisi ya Mtendaji, wakaorodhesha majina ,na kwamba zoezi hilo lifanyie hadi siku ya Alhamisi 12/07/2018 ,kasha Mtendaji apeleke orodha hiyo ya majina wilayani siku hiyohiyo ya alhamisi ili aweze kulifuatilia suala hilo kwa karibu, wananchi hao waweze kurejeshewa fedha zao.
Kuhusu kero ya maji Mhe. Papian ameahidi kushughulikia kero hiyo kuhakikisha kwamba huduma ya maji inasogezwa karibu ,ili wanakijiji hao waondokane na kadhia hiyo. Na kwamba atazungumza na wazabuni wanaoleta maji kwa magari katika kijiji hicho ili kuona ni namna gani bei ya maji itapunguzwa ili wanakijiji hao wasiendelee kununua maji kwa gharama kubwa kama ilivyo sasa . Huku akiendelea na mchakato wa kushughulikia tatizo hilo.
Kwa upande wa kero ya wafugaji kuchungia katika mashamba Mhe. Papian amemuagiza Mtendaji wa kijiji hicho kwa kushirikiana na afisa ugani kushughulikia suala hilo kuhakikisha kwamba tathmini ya haki inafanyika, waliochungiwa mifugo katika mashamba yao wanalipwa fidia, na kwamba wahakikishe pia ushuru wa halmashauri unalipwa wakati wa ulipaji wa fidia hizo.Vile vile amemuagiza mwenyekiti wa kijiji hicho kwa kushirikiana na mtendaji wa kijiji kuhakikisha kwamba mpango wa matumizi bora ya ardhi unazingatiwa na kuheshimiwa na kila mtu.Na kwamba wafugaji walioweka maboma ya mifugo katika maeneo ya kilimo waondoke maramoja, ili tatizo la mifugo kuchungiwa kwenye mashamba lisiwepo tena. Pia majina ya wafugaji wote wanaochunga mifugo kwenye mashamba ya wakulima yaorodheshwe, na orodha hiyo itakabidhiwa kwa mkuu wa mkoa wa Manyara kwa ajili ya hatua kali zaidi .
Mhe. Papian yuko katika ziara ya kukagua miradi ya maendeleo na kuzungumza na wananchi katika vijiji mbalimbali jimboni mwake. Ziara hiyo inafanyika kwa muda wa siku saba,ambapo katika siku ya kwanza ya ziara yake hiyo miongoni mwa vijiji alivyovitembelea ni kijiji cha Mbigiri .
.............MWISHO............
Kibaya-Kiteto
Anwani ya Posta: P.o.Box 98, Kibaya-Kiteto
Simu ya Mezani: +255 027-2552099
Simu ya kiganjani:
Barua Pepe: ded@kitetodc.go.tz
Hakimiliki@2017 Halimashauri ya Kiteto.Haki zote zimehifadhiwa