Mkuu wa wilaya ya Kiteto Mhe Tumaini Magessa akikagua Kitabu cha mahudhurio ya watumishi wa hospitali ya wilaya ya Kiteto wakati wa ziara yake hospitalini hapo mchana wa leo.
.....HABARI KAMILI......
Mkuu wa wilaya ya Kiteto mheshimiwa Tumaini Magessa amefanya ziara ya kushtukiza katika hospitali ya wilaya ya Kiteto, ambapo amekagua idara ya wagonjwa wa nje(OPD), wodi ya wanaume, wodi ya wanawake ,wodi ya watoto,wodi ya wazazi, kliniki ya magonjwa sugu yasiyo ambukiza (sukari, shinikizo la damu na magonjwa ya akili) ,kitengo cha matibabu ya wagonjwa wa bima ya afya (NHIF) pamoja na kitengo cha dawa na vifaa vya tiba.Ziara hiyo imefanyia leo tarehe 28/03/2018 majira ya mchana.
Akiwa katika idara ya wagonjwa wa nje, Mhe. Magessa amekagua kitabu cha mahudhurio ya watumishi wa hospitali hiyo ,ambapo amebaini kuwa watumishi 16 wamechelewa kuingia kazini .Kufuatia uchelewaji huo Mhe. Magessa amesema “ Watumishi 16 wamechelewa kufika kazini leo . Hapa mnahusika na maisha ya watu,lazima umakini uwepo. Msimamizi wa hospitali nitafuatilia kujua ni hatua gani mmewachukulia watumishi hawa. Nataka kuona watumishi hawa wakichukuliwa hatua.Watumishi wawahi kazini, na sio kuwahi tu, wawepo kwenye maeneo yao ya kazi, na wafanye kazi ’’.
Kadhalika katika kitengo cha matibabu ya wagonjwa wa bima ya afya Mhe. Magessa amewataka watumishi wa kitengo hicho kuwa na lugha nzuri kwa wagonjwa ili kupunguza malalamiko ambayo yamekuwa mengi kutoka kwa wagonjwa wanaopata huduma za matibabu kwa kutumia bima.Mhe. Magessa amesema ‘‘Ninyi mnafanya kazi ya uuguzi, katika kazi hii mnahudumia watu ambao wanakuja hapa wakiwa na matatizo makubwa kuliko mnavyofikiria.Kauli zenu zinatakiwa ziwe nzuri, kauli zinapokuwa mbaya, wagonjwa wanapokuja hapa wanaongeza shida zaidi ya zile walizokuja nazo’’.
Katika kitengo cha dawa na vifaa vya tiba , Mfamasia wa wilaya ya Kiteto Mfamasia Mohamed Temba amemueleza Mkuu wa wilaya changamoto kubwa inayowakabili katika kitengo hicho,ambayo ni MSD kutokuwa na baadhi ya dawa na vifaa vya tiba , ambapo wamekuwa wakiagiza dawa na vifaa vya tiba hivyo mara kadhaa lakini hawaletewi. Kufuatia changamoto hiyo ,Mhe. Magessa amewataka watumishi wa kitengo hicho kuandaa orodha ya dawa na vifaa vya tiba vyote ambavyo upatikanaji wake MSD umekuwa ni changamoto ili aweze kulitafutia ufumbuzi suala hilo katika ngazi zinazohusika.
Aidha Mhe. Magessa amewataka madaktari walioko katika kliniki ya magonjwa sugu yasiyo ambukiza ( sukari , shinikizo la damu na magonjwa ya akili) kuelekeza nguvu katika kuelimisha zaidi juu ya namna ya kuishi ili kuepuka magonjwa hayo ,badala ya kushughulika na wagonjwa pekee ,kwani kufanya hivyo hakuwezi kupunguza ukubwa wa tatizo,lakini wananchi wakielimishwa idadi ya wagonjwa kwa siku za usoni itapungua.
Katika ziara hiyo Mhe. Magessa ameambatana na kamati ya ulinzi na usalama . Hata hivyo ziara hiyo sio ya kwanza kwa Mhe. Magessa, kwani amekuwa akifanya hivyo mara kadhaa katika maeneo mbalimbali wilayani Kiteto.